Tuwasiliane-Lets communicate

jokitime@gmail.com

Tuesday, April 30, 2013

VIDEO YA MAQUIS DU ZAIRE YA CHINYAMA , ENZI ZAO

Hawa ndio Maquis Du Zaire, wimbo huu, Kasongo, ulimletea matatizo sana King Kiki ambaye ndiye aliyeutunga, maana serikali yake ya Kongo wakati huo Zaire ikiwa chini ya Mobutu Sese Seko iliuchukulia kama ni fumbo fulani la kisiasa. Hii ilitokea kutokana na kuwa upande wa nchi anakotoka Kiki, kulikuwa na upinzani wa daima na serikali ya Mobutu, japo mwenyewe Kiki anadai wimbo huu haukuwa na uhusiano wowote na matatizo ya nchi yake.  -->
Hapa wanaonekana vigogo kama Chinyama Chiyaza (Baba yake Elly Chinyama), Adios, Viking Nguza, King King, Kanku Kelly, Banza Mchafu na nyota wengine wengi wa miaka hiyo. Mungu awalaze pema wote waliotangulia mbele ya haki


Friday, April 26, 2013

MASHINDANO YA BENDI BORA 1973

Mshindi alikuwa Sunburst aneonekana ni James Mpungwe kiongozi akiwa amevaa kofia, bendi ya pili ilikuwa Tonics na Marijani Rajabu akiwakilisha Safari Trippers iliyochukua zawadi ya tatu

Wednesday, April 17, 2013

BI KIDUDE AFARIKI DUNIA...HISTORIA YAKE FUPI


Mwanamuziki mkongwe katika Taarab Fatuma Bint Mbaraka maarufu kwa jina la  Bi Kidude amefariki dunia muda mchache uliopita huko Bububu Zanzibar, sehemu alikokuwa anaugulia kwa kipindi sasa. Mwili wake utahamishiwa kwake Rahaleo na mazishi yatakuwa kesho. Bi Kidude alizaliwa katika kijiji cha Mfagimaringo, alikuwa binti wa mchuuzi wa nazi, hakuna anayejua haswa Bibi huyu alizaliwa tarehe ngapi, kuna hata mawazo kuwa alikwishafikisha miaka 102.
 Katika mwaka 1920 tayari alikuwa amekwisha anza kuimba katika vikundi vya sanaa kule kwao, mwaka 1930 alijiunga na Egyptian Musical Club ya Dar es Salaam na kuzunguka miji mingi ya Tanganyika wakati ule , mwaka 1940 alirudi Zanzibar ambako awali alikuwa amekimbia kwa kuwa aliozwa kwa nguvu na mtu aliyemzidi sana umri.
Bi Kidude pia liwahi kuimba na Sitti Binti Sadi wakati wa ujana wake, na katika maisha yake Bi Kidude amekwisha zunguka mabara yote akiimba katika majukwaa na wanamuziki maarufu ulimwenguni
Mungu Amlaze Pema Peponi Bibi yetu. Amen

Sunday, April 14, 2013

FELIX MANUAKU WAKU..BABA YA WAPIGA SOLO WA KONGO WA KIZAZI KIPYA

FRANCO
FELLY
Namuheshimu sana marehemu Franco, lakini nadhani kama kuna mpiga gitaa aliyetoa mchango mkubwa sana katika muziki wa Congo katika miaka ya 70 na 80, nae ni mpiga solo Felix Manuaku.  Félix Manuaku Waku, ambaye hujulikana kama Pépé Fely au Felly ni mpiga gitaa kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Huyu bwana alipewa sifa ya kuwa mwanzilishi wa staili ya upigaji wa solo ambao ni maarufu katika upigaji wa muziki ulioko katika mahadhi ya Soukus. Felly alikuwa mmoja wa wanamuziki waanzilishi wa kundi lile maarufu la Zaiko Langa Langa, huku akaanzisha style ya upigaji wa solo wenye spidi kali vidoleni, staili ambao wapigaji kama Diblo Dibala(Machine gun), walikuja kujulikana sana kwa staili hiyo na kwa sasa ndio inatawala katika muziki wa staili ya Sebene. Kutokana na umahiri wake mkubwa wakupiga katika style iliyokuwa ngumu ya kutokuacha nafasi kati ya kipanda na kipande alipata sifa ya kuwa mwanamuziki mwenye ‘MKONO WA SHOTO MGUMU ZAIRE nzima. Mwaka 1979 Felly aliacha Zaiko na kuanzisha kundi jingine matata la Grand Zaiko Wawa. Hebu angalia na  kusikiliza kazi zake katika video hizi 

Baada ya kuweka picha ya Franco akiwa kijana,  mdau mmoja wa blog hii ametuletea taarifa hii..................



Sunday, April 7, 2013

KUMBE NYOTA NDOGO NI MTOTO WA MWANAMUZIKI WA JAMHURI JAZZ BAND

-->
Mzee Abdallah Hatibu (katikati)
Nyota Ndogo  ni jina maarufu sana Afrika Mashariki, ni mwanadada mwanamuziki wnenye sauti tamu sana, kati ya vibao vyake vyote nikiri kuwa wimbo wake wa Watu na Viatu ambao ulishinda tuzo katika Tanzania Music Awards 2007 ni wimbo ninaoupenda sana, pia huyu binti ambaye amekwisha toa album kadhaa zikiwemo Chereko, Nimetoka Mbali na Mpenzi alizaliwa 1981 na akapewa jina la Mwanaisha Abdallah.

Mwanaisha alizaliwa Mombasa  hakumaliza shule na katika kazi alizopitia ni msaidizi wa nyumbani. Katika kuonyesha tena kuwa wanamuziki wengine, muziki umo kwenye damu, baba wa binti huyu alikuwa mwanamuziki. Katika maelezo ya rasmi ya Nyota Ndogo baba yake alikuwa mwanamuziki wa bendi moja wapo Mombasa na aliitwa Abdallaha Hatibu.  Blog ya www.wanamuzikiwatanzania.blogspot.com ambayo ni maarufu kwa kutafiti historia ya wanamuziki wa zamani wa hapa nchini iliweka historia fupi ya kundi maarufu la Jamhuri Jazz Band, pamoja na picha ya mmoja wa wanamuziki wa bendi hiyo aliyeitwa Abdallah Hatibu. Mwanamuziki mahiri Profesa Abbu Omari aliyeko Japan ambaye pamoja na bendi nyingi alizopigia pia alipiga Les Wanyika, na Simba wa Nyika alikuwa na maelezo ya ziada kuhusu Mzee Abdallah Hatibu. Haya ndiyo aliyoyasema……Mkuu Kitime katika picha za hawa wakongwe wa Jamhuri jazz hapo kati kati kuna mwanamuziki alikuwa anaitwa Abdallah Hatibu, sisi tulikuwa tunamjua kama mzee Abdallah,alikwisha fariki miaka kama mitatu iliyopita,Huyu ni baba wa waanamuziki wawili mashuhuri wa Mombasa mmoja msichana Nyota ndogo na mvulana Juma Tutu, Mzee Abdallah alizikwa kwao Muheza baada ya kuishi Mombasa na Nairobi kwa miaka mingi,hata mimi niliwahi kuishi nae jengo moja Nairobi 1982, Mzee huyu alikuwa mkali kwa gitaa nadhani hata kushinda Michael Vicent, nadhani huenda ikawa yeye ndiye aliyemfundisha Michael kupiga gita, niliwahi kumuuliza kuhusu huyu Michael na akasema huyo alikuwa mtoto mdogo tu ki miziki kwake. Kwa kweli huyu mzee Abdallah alikuwa mkali sana kwa gitaa Mombasa nzima na Nairobi alijulikana. …..Abbu Omar Tokyo,Japan

Juma Tutu
Nyota Ndogo
Pia kadri ya website ya Juma Tutu ,                                              (JUMA TUTU)       familia yao walizaliwa sita sehemu ya Majengo huko Mombasa, baba yake alikuwa mpiga gitaa la solo katika bendi ya Simba wa Nyika katika Club ya Sabasaba pale Mombasa, mama yao Christine Mungala pia alikuwa muimbaji katika kwaya ya kanisani. Dada zake wawili Nyota Ndogo na Leila pia ni wanamuziki mahiri.


Wednesday, April 3, 2013

UNAUKUMBUKA WIMBO BB69? SIKILIZA HAPA


Ngaiyaoo Ngaiyaoo
Unipe mama, roho yangu
Nifurahi nayo, mpenzi wangu
Lakini sipendi kuchelewa bure
Wimbo huu nilipousikia mara ya kwanza kupitia santuri ulinigusa mahala ambapo mpaka leo umeacha nafasi fulani. Wimbo huu ulitungwa na Jeannot Bombenga na ukapigwa na na African Jazz group, African Jazz wakati huu ilikuwa imekimbiwa na yule mwamba wa muziki Afrika Grand Kalle ambae aliondoka na kundi Volcan Ni Beto Ba kwenda Ufaransa. Ilikuwa ni kama alama kuwa African Jazz ilikuwa inaweza kuendelea hata bila Mzee Kalle, huyu asije changanywa na Pepe Kaleni watu wawili tofauti sana.