Tuwasiliane-Lets communicate

jokitime@gmail.com

Advert

Tuesday, May 22, 2012

Mwanamuziki wa zamani John Mbula anaumwa anahitaji msaada


Waraka huu nimetumiwa na mwanamuziki mahiri Benno Villa Anthony.................Mkuu, kwanza kabisa namwomba Mwenyezi Mungu akujalie roho ya uvumilivu ktk kufuatilia taarifa hii. Itakumbukwa kuwa mwanzoni mwa mwaka huu, nilikuwa na kipindi cha mahojiano na Manju wa muziki na mtangazaji wa TBC, komredi Masuud Masuud. Kwa vile kipindi kilirudiwarudiwa na huku Manju akitamka namba yangu ya simu, wengi waliinukuu, na kati ya hao walioinyaka ni Mzee John Mbulla, aliyekuwa mpiga sax wa Atomic Jazz. Mzee huyu kwa sasa kweli anaumwa sana. Zaidi ni maradhi ya macho, haoni. Kumbe kwao ni Mpwapwa ila kwa sasa anahifadhiwa na diwani wa Kibaigwa, Ndugu Richard Kapinye.......0717  303070. Baada ya kusikia kuwa wasanii wanachangiana ili kupata tiba, Diwani huyo alinipigia na nikazungumza nao wote wawili. Wameniomba nikupe taarifa hii ili uitoe kwenye vyombo vya habari, ikiwezekana apate msaada wa tiba. Diwani anasema kuwa John akipata operation ya macho atapona na kuanza kujitegemea maana nguvu bado anazo. KUMBUKA...Mzee John Mbulla ndiye aliyepiga Saxaphone kwenye wimbo wa "TANZANIA YETU NDIYO NCHI YA KUSIFIWA", wakati Mbaraka Mweshehe alipojiunga na Atomic Jazz  kwa muda..............Mkuu Kitime, Nina uhakika kama wana Media wakimtembelea na kutoa habari zake, naamini wengi wataguswa na kumsaidia.  Natanguliza shukrani zangu za awali. Asante Mkuu. 

Monday, May 21, 2012

Staying Alive wa BeeGees


Robin Gibb wa BeeGees afariki dunia kwa kansa




Marehemu Robin Gibb
Baada ya kifo cha Donna Summer ( Desemba 31,1948-May 17, 2012), wiki iliyopita,ulimwengu wa muziki umepata pigo jingine baada ya Robin Hugh Gibb, mwanamuziki wa kundi maarufu la BEE GEES kufariki dunia Jumapili 20 May 2012, Robin  alizaliwa tarehe  22 Desemba mwaka 1949. 
Kundi la Bee Gees lilianzishwa kwa pamoja na pacha wake Maurice na kaka yao Barry, japo Robin ndie aliyekuwa maarufu zaidi katika kundi hili. Wazazi wao walikuwa Waingereza japo kwa kipindi fulani walihamia Australia. Inasemekana kundi hili ndilo lililokuwa na mafanikio kuliko kundi lolote jingine la Pop duniani. Kwa karibu miongo 6 kundi hili limekuwa jukwaani, likifanya maonyesho. Kundi liliweza kuuza zaidi ya santuri milioni 200.

 Watanzania wengi walianza kuwafahamu baada ya kusikia vibao vyao kama Staying Alive, Night Fever, How deep is your love na kadhalika  katika filamu ya filamu ya Saturday Night Fever. 

Tarehe 20 May 2012 Robin amefariki baada ya matatizo ya muda mrefu ya kansa ya utumbo. Pacha wake Maurice alifariki kw tatizo hilohilo 2003.

Grammy Awards ambazo kundi hili lilipata:

 1977 Best Performance by a Group — "How Deep Is Your Love"
1978 Best Performance by a Group — "Night Fever"
1978 Album of the Year — "Saturday Night Fever"
1978 Producer of the Year — "Saturday Night Fever"
1978 Best Arrangement of Voices — "Stayin' Alive"
2000 Lifetime Achievement Award
2003 Legend Award

Thursday, May 17, 2012

Donna Summer Hatunae Tena


LaDonna Adrian Gaines  aliyejulikana zaidi kwa jina la Donna Summer amefariki leo Key West Florida akiwa na umri wa miaka 63. Donna Summer amefariki kwa tatizo la Kansa. Donna alizaliwa tarehe 31 December 1948.

LaDonna alikuwa mmoja wa watoto saba katika familia yao iliyokuwa inaishi Boston, Marekani. Mwaka 1971 Donna akahamia Austria ambapo alikutana na Helmuth Sommer ambaye walicheza wote sinema ya Godspell, na wakaoana 1973 walipata mtoto mmoja lakini ndoa ilivunjika 1975. Donna alichukua jina la huyo mumewe aliyekuwa Mjerumani na kulitafsiri jina kwa Kiingereza na akapata jina la Summer ambalo ndilo lilikuwa jina lake la jukwaani. Mwaka 1978 wakati anatayarisha kibao cha ‘Heaven Knows’ ndipo alipokutana na Bruce Sudano na wakaoana July 16, 1980, japo 1979 walipata mtoto wao kwanza, mtoto wa pili alizaliwa 1981.

Pamoja na nyimbo zake kuigwa na wanamuziki wengi kama Madonna, Whitney Houston, Diana Ross, Britney Spears, kwa mfano ule wa "Love to Love You Baby" ulikuwa sampled na Beyonce Knowles na unajulikana kama "Naughty Girl", Donna alikuwa na rundo la awards na mafanikio mengine, kati ya awards alizopata ni;

  • NAACP Image Award
  • Juno Award nomination kwa Best Selling International Single,"I Feel Love"
  • Multi-Platinum album 3 katika Marekani
  • Album zake 11 zilipata Gold nchini Marekani
  • Gold singles 12
  • American Music Awards 6
  • Alikuwa mwanamke wa kwanza Mmarekani mweusi kupata MTV Video Music Awards
  • Golden Globe Awards 2
  • Donna Summer aliweza kupata jumla ya Grammy Awards 5
  • Na aliwahi kuteuliwa mara 12 kwa ajili ya Grammy Award

Alipata heshima nyingine nyingi tu



Tulio cheza muziki wako tutakumiss Donna,

 Nakumbuka Love to love you baby, Bad Girls, I feel love na kadhalika


Monday, May 14, 2012

Mjue Issa Juma aliyeimba Sina Makosa


Issa Juma Singano alikuwa muimbaji, wengi inakuwa rahisi kumfahamu nikisema  yule muimbaji aliyeimba wimbo wa Sina Makosa. Issa alizaliwa Tanga, alianza muziki akiwa na umri wa miaka 15.Alianza muziki huko kwao Tanga na moja ya vikundi vingi vilivyokuwepo Tanga wakati ule, na akweza kwenda hadi Uganda ambako alikaa mpaka 1970 alipoingia Dar es Salaam na akajiunga na Police Jazz ya Dar es Salaam, miezi sita baadae akahamishiwa Police Jazz ya Tanga. Uwezo wake wa kuimba ukavuka mpaka hadi Kenya na kusikika na producer maarufu A.P. Chandarana, huyu akamuita Issa Juma Kericho. April 1971 Issa akahamia Kericho na kujiunga na Kericho Jazz Band, bendi haikudumu muda mrefu ikasambaratika na Chandarana akamuajiri Issa kama recording assistant kwenye studio yake maarufu ya Chandarana. Issa aliishi sana hapa hata kuanza familia yake hapa. Alijaribu kurekodi nyimbo zake kadhaa lakini hazikupata umaarufu. Mwaka 1977 akaamua kuhamia Nairobi. Alipofika Nairobi akajiunga na Orchestra Kumbakumba ambayo ilikuwa na mchanganyiko wa wanamuziki wa Tanzania na Kenya, mmojawapo akiwa mwanamuziki maarufu muimbaji wa Jamuhuri Jazz band Yusuph Mhando. Mwishoni mwa mwaka 1978 Issa Juma akajiunga na Simba wa Nyika. Kama ilivyohadithia katika makala zilizopita Issa alifika Simba wa Nyika akaikuta katika mgogoro mkubwa ambapo wanamuziki wengi walikuwa wakijiandaa kuanzisha Les Wanyika. Nae akawa mwanamuziki muanzilishi wa Les Wanyika. Na hapa ndipo sauti yake ilikuja kujulikana sana katika ile album iliyokuwa na nyimbo kama Sina Makosa, Pamela, Paulina na kadhalika. Aliacha Les Wanyika June 1981 na kwenda kujiunga na Super Wanyika. Mwaka 1988 alipata ugonjwa wa kupooza na akafariki mwishoni mwa mwaka 1990. MUNGU AMLAZE PEMA PEPONI.

Sunday, April 15, 2012

Abbu Omar Profesa Omar Junior


Ganda la album ya 3 ya Abbu Omar
Abbu Omar Njenga, mwanamuziki ambaye ndiye ambaye amenipa historia nzima hii ya Simba wa Nyika, alijiunga rasmi na Simba wa Nyika 1981, mwaka ambao aliingia Nairobi kupitia Mombasa akitokea UDA Jazz. Nia yake ya awali ya kwenda Kenya ilikuwa ni kutafuta elimu zaidi baada ya kuwa amemaliza Songea Boys high School, aliona kwenda Kenya angeweza kupata chuo ambacho kingeweza kumpa elimu ambayo ingemnyooshea maisha. Bahati mbaya alikuta ada zilikuwa juu kuliko uwezo wake, hivyo akalazimika kutafuta kibarua ili aweze kuishi. Kazi ambayo ilikuwa rahisi zaidi kupata ni kazi ya muziki kwani alikuwa na kipaji cha kupiga muziki na alikuwa mwanamuziki wa UDA Jazz 'Wana Bayankata'. Alimwendea mwanamuziki Charles Ray Kasembe wa Les Volcano ili ajiunge na bendi hiyo. Huyu Charles Kasembe ndiye aliyekuwa mpiga rhythm gitaa wa Mbaraka Mwinyshehe wa muda mrefu(nyimbo kama Wajomba Wamechacha) aliacha Super Volcano kabla ya kifo cha Mbaraka na Mbaraka akampata mpiga rhythm mwingine aliyeitwa Stanley Mtambo aliyedumu mpaka kifo cha Mbaraka.
Kutokana na kuwa mpiga gitaa maarufu wa Super Volcano Charles Kasembe aliona ni heri kuanzisha bendi  aliyoiita Les Volcano.  Abbu hakupata nafasi Les Volcano maana ilikuwa imeshajaa wanamuziki. Kasembe alimshauri Abbu awaone Wilson na George Peter ambao wakati huo walikuwa katika jitihada za kufufua tena Simba wa Nyika. Charles mwenyewe alimpeleka Abbu mpaka Bombax Club  iliyoko Ngong Road, ambapo ndipo Simba wa Nyika walikuwa wanajiandaa kupiga. Abbu alipandishwa jukwaani siku hiyohiyo na kukabidhiwa gitaa la rhythm, upigaji wake ukampa kazi siku hiyo hiyo.  Kwa hiyo pia Abbu akashiriki katika album ya kwanza ya awamu hiyo ambapo album hiyo ilikuwa na nyimbo kama Barua ya Mapenzi, Mama Nirudie,  na palikuweko album nyingine na ikafuata album ya tatu iliyokuwa na ule wimbo maarufu wa Shilingi  Yaua, Abbu alikaa Simba wa Nyika mpaka 1987 ambapo aliacha bendi, lakini aliendelea kuwa na uhusiano na bendi hiyo na kuendelea kushiriki katika recording mbalimbali za bendi hiyo  hadi ya mwisho 1992 kabla ya kifo cha George Peter. Abbu Omar ambaye kwa upigaji wake wa rhythm ulimfanya arith heshima ya Professsor Jnr ikikumbukwa kuwa Professor Omar mkubwa alikuwa ndiye yule aliyeanzisha Les Wanyika. Kwa sasa Abbu Omar yuko Japan ambako ana piga muziki mara nyingine kwa kushirikiana na Fresh Jumbe na Lister Elia

Wednesday, April 11, 2012

Kupukutika kwa Super wa Nyika na kuzaliwa Orchestra Vinavina



Mwishoni mwa mwaka 1981 ndipo Issa juma alipoamua kujitoa Les Wanyika. Sauti yake ilikwishakuwa maarufu kutokana na nyimbo alizoimba akiwa bendi hiyo. Maproducer kutoka kampuni mbalimbali za kurekodi mjini Nairobi waliposikia hilo wakaanza kumfuata ili arekodi katika studio zao. Kampuni iliyoweza kumpata ilikuwa na kampuni ya Meghs iliyokuwa mali ya mhindi mmoja aliyejulikana kwa jina la Babuu. Katika kampuni hiyo alirekodi nyimbo kadhaa zilizokuja pata umaarufu. Kimsingi inaoneka mwanzoni Issa hakuwa na wazo la kuanzisha bendi, mpaka alipolazimika kutafuta jina  la bendi ya kuzibeba nyimbo hizo alizorekodi, ndipo kwa mara ya kwanza jina la Super Wanyika lilipozaliwa. Nyimbo zilizotolewa kwa jina la bendi hii zilikuwa  kama Anita, Unataka nikupendeje, Jennifer na kadhalika. Wanamuziki walioshiriki katika kazi hizi za mwanzo walikuwa Mohamed Tika, Shoushou Batenga, na Michael Beche waimbaji, huyu Mzee Shoushou alikuwa Mkongo ambaye  aliwahi kupitia bendi ya safari Trippers. Mzee Maneno Shaaban alipiga drums, Issa Khalfani Bendera, kwenye solo, Stanley Mtambo gitaa la rhythm, George Madrago gitaa la bezi, Said Makelele na  Mambi Iddi wakiwa kwenye trumpet. Nyimbo zilipotoka zilianza kuvuma na kulazimisha bendi ianze kufanya maonyesho. Wanamuziki wakakubaliana na Babuu ambae pamoja na kuwa na studio pia alikuwa na vyombo vya muziki, hivyo akawakodisha vyombo hivyo kwa mkataba maalumu. Super Wanyika ilidumu kwa zaidi ya muda wa miaka mitatu. Baadhi ya wanamuziki waliokuwemo katika kundi hilo ni Mzee Mohamed Tungwa akipiga solo, Abdalah Kimeza kwenye Saxaphone, Jumanne Kilongola kwenye trumpet, Joseph Tito akipiga gitaa la rhythm, Shwaib Ole monduli muimbaji, na wengineo. Lakini bendi hatimae ilikuja kufa kwa makosa yaleyale ya uongozi mbovu. Issa Juma akaanza kusahau kuwapa wanamuziki wenzie haki stahili. 
Sauti yake iliendelea kuwa muhimu katika anga la muziki, hivyo akaanza kuingia mikataba tofauti na ule aliyokuwa nao Meghs. Akaingia mkataba na kampuni ya AIT, halafu akaingia mkataba na producer mashuhuri Nairobi wakati huo Bwana Joe Mwangi wa Matunda Production. Sasa kazi ambazo zilifanywa katika mikataba hiyo mipya alitambulisha kuwa zimerekodiwa na bendi aliyoitambulisha kama Wanyika Stars, baadhi ya nyimbo ambazo zilirekodiwa kwa jina hilo ni kama  Sigalame,Mpita njia,Bomanga, Mony na kadhalika. Kutokana na wanamuziki hawa walioshiriki kazi hizi, baadhi wakaunda kundi la Sigalame System ambalo halikudumu sana, wengine wakaunda kundi la Orchestra Vinavina, pamoja na kuwa na muziki mzuri hawa Vinavina hawakuwa na bahati ya kupendwa hivyo wakaondoka Nairobi na kuhamia Morogoro Tanzania, wengi wa wanamuziki wa bendi hii asili yao ilikuwa Morogoro,baadae bendi hii ilikuja kuitwa Les Cubano.  Les Cubano ilikuwa na wanamuziki kama Michael Beche, Niko Zengekala, Shwaib Ole Monduli, Banza Tax wakiwa ni waimbaji, Mohamed Tungwa na Issa Bendera wapiga solo,Fred Mwalasha rhythm gitaa, George Madrago gitaa la bezi, Mzee Maneno Shaaban akipiga drums, Said Makelele, Mambi Idd, Jumanne Kilongola wapiga trumpet, Kibwana Magati alikuwa anapiga drum na bezi, Abdalaah kimeza na Comson Mkamwa walikuwa wapuliza sax.......itaendeleaaa